Viazi vitamu ni moja kati ya mazao ya mizizi yanayolimwa kwa ajili ya chakula cha binadamu na mifugo. Pia ni kwa ajili ya malighafi viwandani na kuongeza kipato kwa mkulima. Zao hili ni muhimu kwa ajili ya usalama wa chakula katika kaya kwa kuzingatia uvumilivu wa ukame na uzalishaji wa kuridhisha wa mazao ambayo ni mizizi yake na ndiyo chakula chenyewe. Viazi vinalimwa karibu maeneo mengi ya nchi ya Tanzania yenye hali ya hewa tofauti, mfano Kagera kuna mvua nyingi lakini viazi vinastawi, kanda ya kati mvua chache lakini viazi vinastawi na ndio wazalishaji wakubwa ikiwemo Dodoma na Singida. Viazi vinashika nafasi ya tano kwa mazao ya chakula hapa nchini baada ya Mahindi Muhogo, Mpunga na Mtama, lakini kwa mazao ya mizizi ni la pili baada ya Muhogo. Viazi vitamu vina faida nyingi kuanzia majani hadi mizizi kama tutakavyoona baadae.